Thursday, March 6, 2014

STEVEN M. WASSIRA NA Mbio za URAIS.....!!


 

.......HII IMETOKA KWENYE MTANDAO WA JF;.......

Stephen Masato Wasira si jina geni kwa Watanzania, ni jina maarufu. Umaarufu wa Wasira ambaye kwa sasa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu unatokana na mambo mengi.

Haya ndio yamenifanya nianzishe mpango maalum wa kumchunguza kihabari ili niwaoneshe Watanzania upande mwingine wa shilingi kuhusu Mwanasiasa huyo, lakini nakiri kuwa “nimeshindwa kumpata” Wasira katika hilo.

Huyu ndiye Wasira ambaye Mwaka jana aliwatahadharisha Vijana wasomi wa Vyuo Vikuu kutumia taaluma zao kupambanua ukweli na uwongo wa vyama vya siasa ili wasiendelee kuwa wateja wa siasa uchwara na “wachumia matumbo”

Nimeshindwa kumpata WASIRA aliyeyasema hayo katika kongamano lililofanyika mkoani Mwanza na kushirikisha vyuo mbalimbali mkoani humo kikiwemo Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine Tanzania(SAUT).
Nimeshindwa kumpata kwani kati ya watu niliobahatika kuzungumza nao au niliosoma mandishi yao, hakuna aliyenipa kashfa hata moja inayomgusa Wasira tofauti na upungufu wa kawaida ambao hakuna mtu wa kawaida duniani anayeweza kuukosa.

Baada ya juhudi zangu kushindikana kumpata Wasira ndipo najiuliza “HUYU WASIRA NI MTU WA NAMNA GANI?”
Katika kumtafuta Wasira na dosari zake, nakumbana na Gazeti la Raia Mwema Toleo la 2677 la November ,2013 likiwa na kichwa cha habari kisemacho “Nani ni nani CCM?”

Katika Habari hiyo Gazeti linasema “Stephen Wasira anatajwa kuwa ni mwanasiasa mwenye uwezo wa kuendesha siasa za jukwaani, lakini pia ni mwanasiasa mwenye kupenda siasa za suluhu miongoni mwa wanachama wa CCM, akiwa pia mwiba kwa upande wa vyama vya upinzani kwa wepesi wake wa kujibu mapigo”

Linaongeza”Ingawa CCM haijawahi kuonja historia ya kuwa chama cha Upinzani lakini Wasira amewahi kuingia upinzani na kushinda uchaguzi wa ubunge kupitia NCCR-Mageuzi, akimbwaga aliyepata kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Jaji Joseph Warioba”.

Christopher Gamaina, Mhariri wa Gazeti la Jamhuri , anamtaja Wasira akisema “Sifa moja kubwa anayotajwa kuwa nayo Wasira ni usafi wa kimaadili ndani na nje ya Chama chake (CCM) kwa maneno na matendo ya maisha yake”.
Gamaina anasema ,“ Pia Wasira anatajwa na watu wengi kwamba ni mtu mwenye msimamo imara katika vita dhidi ya Ufisadi ndiyo maana hana doa wala kashfa ya ufisadi, lakini kubwa zaidi anatajwa kama mmoja wa makada wenye utashi na ushawishi mkubwa wa kisiasa ndani ya CCM na mwenye upeo mpana wa kuona mbali”.

Mmoja wa viongozi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Dar es Salaam aliyetoa maoni yake kwa sharti la kutotajwa jina wala cheo, anasema “Ukiachia nafasi walizopata kuwa nazo wenzake, kati ya wanaosemwa (anamaanisha kuutaka Urais mwaka 2015), Wasira ni msafi kuliko wote kwasababu sijawahi kusikia kashfa yake ni mtu mwenye uzoefu mkubwa katika masuala ya siasa na utawala.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa uchunguzi wa makala haya, WASIRA amepata kuwa Mbunge wa Mwibara (mwaka 1970-1975), Bunda (1985-1990),(1995-1996) na (2005-2010). Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010,Wasira alichaguliwa tena kuliwakilisha Jimbo la Uchaguzi la Bunda.

Taarifa zilizopatikana katika mtandao zinasema Wasira pia amepata kuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara (mwaka 1975 hadi 1982) na Mkuu wa Mkoa wa Pwani mwaka 1990 hadi 1991.

Habari hizo za kimtandao zinafahamisha kuwa kati ya mwaka 1982 na 1985, Wasira alikuwa Waziri Mwambata katika Ubalozi wa Tanzania Washngton DC, Marekani na kisha akawa Naibu Waziri wa Kilimo mwaka 1972-1975, na Serikali za Mitaa mwaka 1987-1989.

Kwasasa Wasira ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu) na Mbunge wa Bunda mkoani Mara.
November Mwaka jana , mmoja wa wachangiaji katika mtandao wa Jamii Forum(JF) aliandika kuhusu Wasira akisema “Huyu mzee namkubali sana ,kwanza hana makundi katika chama na mzee huyu namkubali pia katika hotuba zake zenye nguvu na ushawishi. Namkubali sana..”

Alipoulizwa kuhusu anavyowajua makada watatu wa CCM wanaotajwa kuhusu kuwania Urais katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Mwaka 2015, yaani mawaziri wakuu wazamani, Frederick Sumaye, Edward Lowasa na Wasira, Mratibu wa ULINGO ambayo ni ASASI ya Umoja wa Wanawake katika vyama vya siasa vyenye Wabunge katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dr. Ave Semakafu, amesema, “Sijaona yeyote kati ya hao anayejali na kuhudumia kwa dhati makundi ya watu walio pembezoni”.

“Wengi wanafanya siasa kavu tu za kuwapa vijana mipira na jezi, wakati wana matatizo magumu yanayowakabili kimaisha. Mipira sio tatizo la Watanzania . Wengine wanasema vijana wamekalia bomu la ajira, lakini hawaoi jawabu la tatizo hilo”.
Anaongeza, “Rais Jakaya Kikwete ndiye amekuwa Mfano bora kwa kuyajali makundi yote ya Watanznia. Amejitahidi hata kuwa karibu na watu na kuweka usawa wa kijinsia.Mfano amejitahidi kuteua majaji wanawake ; ameonesha mfano wa kuinua vijana na wanawake hata katika ule mfuko ulioitwa “Mabilioni ya Kikwete” na kusidia Vijana kupitia mifuko mbalimbali hadi ngazi ya wilaya.”

“Natamani kumpata Mwanasiasa huyu nayetajwa kuwa jasiri asiyeogopa wala kusita kufanya uamuzi mugumu kwa maslahi ya umma” Na nimwambie kimoja wanachosema watu wanaomsema vizuri kwamba zile chagamoto ambazo hajazishughulikia jimboni kwake Bunda, azifanyie kazi.

Nimejitahidi kumtafuta Wasira kwa siku tatu mfululizo nikabahatika “kumpata” kwenye dosari moja waliyonayo Mawaziri karibu wote wa Kikwete kuwa, hawapendi kupokea simu. Hapo nimempata na kumweka kwenye kundi la wabunge na mawaziri wenzake .

Tuachane na hayo; Nimemtafuta Wasira sikumpata, maana nilitaka nimjulishe kuwa kuna mmoja ameshauri afanye juhudi kubwa n haraka ili kukamilisha ‘juhudi zake’ za kuondoa shida ya maji katika maeneo ya Nyamakokoto,Bunda stoo,Nyasura,Migungani na sehemu nyingine.
 

Bado naendelea “kumtafuta” Stephen Masato Wasira ili nijiridhishe iwapo kweli hana hata kashfa moja kama wanavyosema watu wengi. BADO NAENDELEA KUMTAFUTA.


Makala kwa Hisani ya Gazeti la Pata Habari

No comments :

Post a Comment

 
Copyright © 2013. BongoAfrica - All Rights Reserved.